Na
Seif Mangwangi
MKURUGENZI
wa Jiji la Arusha Dkt John Pima amewataka vijana wanaosimamia zoezi la anwani
za makazi kutojihusisha na mambo ya kisiasa katika maeneo watakayokuwa wanafanyia kazi kwa kuwa kufanya hivyo ni kinyume cha
maadili ya utumishi.
Akizungumza
na kundi la vijana walioteuliwa kwaajili ya kuweka anwani za makazi (post
code), sanjari na kubainisha na kuweka alama na majina ya mitaa katika kata 20
zilizosalia za Jiji la Arusha , Dkt Pima amesema zoezi hilo ni nyeti na linahitaji
uangalifu wa hali ya juu. Tayari Jiji hilo linaendelea na zoezi hilo katika
kata tano za awali.
“Nimekuja
hapa kufungua mafunzo yenu lakini pia kuwaeleza mambo machache ambayo tunayatarajia
kutoka kwenu, sitarajii kusikia miongoni mwenu mmejihusisha na mambo ya kisiasa, lolote mtakalolisikia toeni taarifa kwa msimamizi wako,”amesema.
Amesema
vijana hao wanapaswa kujua kuwa kazi ya Serikali ni kazi ya siri kubwa na hivyo
hatarajii mambo yanayohusika na siri za zoezi hilo yatoke nje ya viongozi wanaosimamia zoezi hilo au yeye mkurugenzi.
Dkt
Pima amewataka vijana hao kufanyakazi hiyo kwa bidii ili kuhakikisha
linakamilika kwa wakati kama ilivyopangwa na Serikali na kwamba endapo
watakutana na vikwazo vyovyote watoe taarifa mapema kwa maafisa wanaowasimamia.
“Tunatarajia
zoezi hili la awali litaisha ndani ya wiki mbili kuanzia kesho Februari 22,
2022, baada ya hapo mtaendelea na zoezi lingine gumu zaidi ambalo ni kuweka
alama ambapo hatua hii umakini zaidi tena unahitajika na ninaamini kwa jinsi
ninavyowaona mnaweza kufanyakazi vizuri sana,”anasema.
Kwa
mujibu wa Mkurugenzi Dkt Pima Jiji la Arusha linatarajia kumaliza zoezi hilo
Machi mwaka huu, huku kitaifa zoezi hilo likitarajiwa kumalizika mwishoni mwa
mwezi Mei 2022.
Kwa upande wake msimamizi wa zoezi hilo katika kata sita ndani ya Jiji la Arusha Ernesta Moshi amesema amepokea maelekezo ya Mkurugenzi kuhusiana na maadili katika kazi hiyo na ameshatoa maelekezo kwa vijana wanaoenda kutekeleza zoezi hilo kuwa makini.